Monday, 9 September 2013

WALEMAVU WANAVYOTESEKA DAR ES SALAAM

Siri nzito ya walemavu wanavyoteseka Dar.

 INASIKITISHA na kuleta huzuni ndani ya moyo wako pale unapojikuta unawapoteza wazazi wako wote huku ukikosa msaada kutoka kwa ndugu wa karibu na kuamua kujiunga na kundi la ombaomba barabarani. Baadhi ya watu wanao kuwa wakiomba msaada hasa wale walemavu wa viungo mbalimbali wa mwili wamekuwa wakileta huzuni kwa wapiti njia kutokana na ulemamavu wao ambao ni mipango ya Mungu. Sote ni mashahidi kuwa baadhi ya walemavu wa mikono, miguu, vipofu na viungo vingine wakiomba msaada kwa madereva, watembea kwa miguu na kwenye ofisi za Serikali na binafsi na maeneno mengine. Lakini wapo wengine ambao hawana tatizo lolote lakini wameamua kuingia katika kundi hilo jambo ambalo limekuwa likizua maswali ya kwamba kwanini wasijishughulishe na biashara ndogondogo. MTANZANIA Jumatatu ilifanya mahojiano na mlemavu mmoja wa miguu yote ambaye amekuwa akitembea mithili ya mnyama mwenye miguu minne wakati akiomba msaada katika kituo cha daladala Ubungo. Mlemavu huyo aliyejitambulisha kwa jina la Yusuph Said (24) mzaliwa wa Kijiji cha Mikese mkoani Morogoro anaeleza maisha anayoishi eneo la Manzese Darajani jijini Dar es Salaam ambayo ni hatari kwa usalama wa uhai wake. Said ambaye alisoma Shule ya Msingi Kitega na baadaye kujiunga na Sekondari ya Mikese zote za mkoani Morogoro anaeleza kwamba alikimbiwa na ndugu zake baada ya wazazi wake wote kufariki 2000 kutokana na maradhi mbalimbali. Akizungumza kwa huzuni ya kuwapoteza wazazi wake ambao walikuwa wanamlea kulingana na hali yake ya ulemavu alijikuta akikosa mtu wa kukaa naye kitendo kilichomfanya kukimbilia kwa shangazi yake Muhombola Salum. Said anasema alikimbilia kwa shangazi yake baada ya ndugu zake wa kuzaliwa tumbo moja kumkimbia na kuanzisha maisha yao maeneo mengina huku shughuli zao kubwa ni kuchoma mkaa porini. Anasema maisha kwa shangazi yake yalizidi kuwa magumu kutokana na kutokuwa na uwezo kwani uhakika wa kula kila siku haukuwapo ambapo alishindwa kuvumilia njaa na kukimbilia Dar es Salaam baada ya kupata taarifa kuwa walemavu wanapata msaada barabarani kwa kuombaomba. Hakika, ukimtazama Said hali yake ni vigumu kuvumilia kumsikiliza au kumwangalia kwani mwili wake unaonekana kutooga siku nyingi, nguo chafu, shuka analojifunika chafu ana anatembea nalo muda wote kwa kuhofia kumwibia. Pia inadhihirisha kabisa ameanza kuathirika kisaikolojia kutokana na mazingira anayoishi na inathihirisha wazi ameanza kutumia dawa za kulevya. Said ambaye alikataa kuweka wazi vitendo wanavyofanyiwa walemavu wanaoishi eneo la Manzese Dar es Salaam nyakati za usiku kwa kuhofia maisha yakwe, anasema anatamani kurudi nyumbani lakini anashindwa wapi atafikia. “Pale Manzese kuna masela wengi sana, wanatufanyia mambo mengi lakini siwezi kuyataja hapa naogopa na ndio maana sisi walemavu tumejitenga na banda letu. “Hii ni shuka ninayojifunika natembea nayo muda wote kwa ukiachaa unaibiwa, kuoga kwangu au kufua nguo hizi mara nyingi ninasubiri mvua inaponyesha. “Mimi nilikuwa nalelewa na wazazi wangu bila kutekeseka na walikuwa wameninunulia baiskeli lakini walipofariki iliharibika na hakuna aliyenitengenezea lakini nashukuru hadi leo naishi kwa msaada wa watu. “Ukiamua kuwahoji wapiga watu tunaolala nje watakueleza mambo mengi sana, kuna vituko tunafanyiwa sio kwmaba tunapenda ni kwa sababu huna jinsi,”anasema kwa masikitiko. Said anasema kwamba kutokana na kukaa kituoni tena juani kwa kuomba pesa abiria, madereva na makondakta amekuwa akiugua kila siku lakini baada ya kupata kiasi hutenga kwa kula chakula na kununua dawa la kutuliza maumivu. Anasema kwamba anahofia kwenda hospitali kutibiwa kwa kile alichodai hatapewa fursa ya kupata matibabu kwa sababu ya pesa na hali yake ilivyo. Anasema kwa siku inaweza kupata Sh 5,000 lakini kutokana na mazingira anayoishi hazitoshi na kuongeza kwmaba pengine hunyang’anywa na masela nyakati za usiku. Anaeleza kwamba mbali ya kunyang’anywa fedha pia kupokonywa simu jambo ambalo linamfanya kutonunua simu, nguo au kutunza fedha za ziada. Anasema kutokana na hali hiyo hulazimika kuchimba shimo na kufukia baadhi ya fedha zake anazopata kutoka kwa watu wanaoguswa na hali yake. Said aliwataja baadhi ya ndugu wa kuzaliwa ni pamoja na Oluka, Salum, Hiari, Shukuru na Hamis ambao wapo porini wakiendesha shughuli zao za kukata miti na kuchoma mkaa mkoani Morogoro. Pamoja na mambo ya Said lakini ombi lake kubw ani kuiomba Serikali kumsaidia baiskeli ya kutembelea au kumpeleka katika kituo chochote za kulelea watu wasio na uwezo. Said anasema mbali ya kumpeleka kituoni, anaomba msaada wa fedha ili kuanzisha biashara ndogo ambazo anaweza kusifanya kwa kutumia mikono ambayo haina ulemavu wowote. Ni dhahiri kwamba Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto inapaswa kutambua matatizo yanayowapata watu wanaojihusisha na ombaomba barabarani. Inagawa ni vigumu Serikali kuwachukua watu wote walio mitaani na kuwatunza lakini kuja haja ya kuchukulia uzito kwa watu wenye ulemavu hata kwa kuwapeleka katika vituo vya kulelea watu wasio na uwezo. Si kwamba walemavu wote wanapenda kukaa kwenye vituo hivyo la hasha, bali wengine wanataka kupata msaada wa fedha ili kuanzisha biashara ambayo wanaweza kuifanya kulingana na mazingira yao. Pia Serikali inapaswa kuweka wazi juu ya huduma kwa walemavu katika hospitali za umma ili waweze kupata huduma bure kwa sababu ya hali zao ambazo haziwawezeshi kupata kipato cha kujikimu, hii itasaidia pale wanapougua walemavu waweze kupata matibabu kwa sababu wana haki sawa. Walemavu wanapoachwa bila kupewa huduma ni moja ya sehemu ya kuwafanyia ukatili. Sote tunafahamu ukatili ni vitendo vya makusudi vinavyofanywa na mtu au kikundi dhidi ya mtu, watu wengine ambavyo huwa na madhara ya kimwili, kiakili na jisaikolojia. Dhana hii haimanishi kuuawa kwa binadamu pekee bali ukatili unaweza kujitokeza katika sura tofauti na maneno mbalimbali kama ukatili wa nyumbani, kiuchumi, kimila na desturi katika makabila, mahusiano ya kimapenzi, usafirishaji haramu wa binadamu, vitisho na matumizi ya kutumia nguvu. Hivyo watu walio barabarani wakiomba msaada wa kusaidia wapo katika kundi la ukatili wa kiuchumi ndio uliowafanya kuingia barabarani kujipatia riziki zao. Kwa mujibu wa Said amesema kwamba nyakati za usiku hufanyiwa vitendo vya ajabu ambavyo hakuta kuvieleza wazi, lakini kwa akili ya kawaida inadhihirisha kundi hilo linateseka sana . Ukatili unaweza kutoka katika kundi lolote ndani ya juamii ikiwa ni kwa mwanamke, mwanaume, mvulana, msichana au mototo. Ili kutambua madhara ya ukatili wa kijinsia kwa walengwa hao ni muhimu kufanya linalowezekana kuhakikisha vitendo hivyo vinatokomezwa kuanzia ngazi ya familia hadi taifa kuona kila binadamu ana haki katika hali yoyote ile. Ingawa mateso wanayopata walemavu barabarani jamii imekuwa ikiyachukulia pengine ni uamuzi wa mtu kupenda kuingia katika kundi hilo lakini sivyo ilivyo bali inalazimu kutokana na hali halisi ya maisha. Umefika wakati sasa wizara, idara, taassi na kampuni binafsi kuona kundi la walemavu ni moja ya watu wanaopaswa kusaidiwa katika kila hali kwa sababu hayo ni mapenzi ya Mungu. Pia vitendo vya baadhi ya familia kuwatelekeza watoto wanaozaliwa kwa ulemavu au kupata ulemavu wakiwa watu wakubwa ni jambo la kikatili , ni vema mlemavu akadhaminiwa kama ilivyo kwa wengine. Maoni 0769 688 300

No comments:

Post a Comment