Wednesday, 19 February 2014

WASOMI WANAPOFANYA UKATILI WA WATOTO WAO



Wasomi wapuuza sheria za watoto na kufanya ukatili
*Mtoto apoteza mikono kisa wizi wa viazi
Na   Benjamin Masese, Mwanza
MWAKA 2009 Serikali kupitia Bunge lake ilipitisha sheria za kuwalinda watoto ambayo ililenga kuweka usalama kwa watoto dhidi ya mazingira hatarishi na unyanyasaji.
Kwa mujibu wa sheria hiyo  inamtaka kila mtu kumtunza na kumlea mtoto katika maadili na makuzi mema bila kumfanyia ukatili wa aina yoyote ile.
Katika sensa iliyofanyika mwaka 2012 inaonyesha watanzania wote  ni zaidi ya  milioni  45 na kati ya hao asilimia 50 ni watoto ambao ni hazina ya taifa la kesho.
Katika sheria hizo za mtoto zimeanisha kanuni muhimu zikiwamo maslahi bora ya mtoto ambaye anapaswa kufanyiwa matendo mema ya msingi ya  kuishi bila ubaguzi, unyanyapaa kwa misingi ya jinsia, umri, asili yake, rangi, dini, hali ya kiafya, ulemavu, desturi, kabila, hali ya kiuchumi na nyinginezo kama hizo.
Sheria  hizo zinaelekeza kwamba  mtoto ana haki ya kuishi na wazazi, walezi na kukua katika mazingira ya amani kwa kupewa matunzo sahihi.
Pia sheria hiyo  inasema ni kosa kwa mlezi au mzazi wa mtoto kushindwa kutoa mahitaji ya msingi kwa ajili ya uhai na makuzi ya mtoto.
Inabainisha kwmaba kitendo cha mtoto kushindwa kupewa mahitaji ya msingi kinamtia hatiani mlezi au mzazi  kwa kutozwa faini  kuanzia Sh 500,000 hadi  Sh milioni au kifungu cha miezi sita hadi miaka mitatu.
Pamoja na uwepo wa sheria hizo lakini vitendo vya ukatili wa watoto wadogo umeendelea kufanyika nchini huku Kanda ya Ziwa ikionekana kuwa ni jambo la kawaidwa.
Ni jambo lisilo la kificho kwamba mikoa ya Kanda ya Ziwa ikiwamo Mwanza, Mara, Shinyanga, Kagera, Simiyu na wilaya zake, vitendo vya ukatili kwa rika zote vimekuwa ni adhabu ya kawaida na   kuonekana ni haki kujeruhi, kuua au kumfanyia mtu ulemavu wa kudumu.
Mikoa hiyo hiyo imekuwa na historia ya vitendo vya ushirikina na  mauaji ya kikatili hali ambayo imebadilisha hadhi ya wakazi ndani ya taifa lao huku jamii nyingine ikiwaona  watu wa kuogopwa  na hatari kutokana na ukatili unaotendeka ndani ya maeneo yao.

“Ni hali ya kushangaza  kuona  wasomi tena waajiriwa wa Serikali katika sekta ya elimu na idara za kusimamia haki, usalama wa raia na mali zake wanakuwa sehemu  au miongoni mwa watu wanaotenda unyama wa kutisha kwa watoto wenye umri mdogo na kuwatelekeza bila matibabu yoyote”
Elfrida Nicholaus (7)  ni miongoni mwa watoto waliofanyiwa ukatili na mlezi wake  na mke wa mjomba wake, Ester Benedict Miti ambaye ni mwalimu wa Shule ya Msingi Sweya na kumficha ndani ya nyumba kwa siku bila matibabu”
Mtoto Elfrida alichomwa mikono na mwalimu Miti  mwaka jana  ambapo alimfunga  kitambaa na kumwagia mafuta ya taa kwa kile kilichodaiwa aliiba viazi vitamu kwa jirani yake.
Mtoto Elfrida alichukuliwa  na mjomba wake Selestine Kasendela ambaye ni  askari polisi wa kituo cha Kirumba Wilaya ya Ilemela  jijini Mwanza  kutoka kwa mama yake mzazi, Marina  Fabian anayeishi mkoani Kigoma.
Askari huyo alimchukua mtoto huyo kwa nia njema kwa lengo la kuja kukaa naye kwa kuwa mazingira aliyokuwa akiishi na mama yake mzazi  yalikuwa mabaya kutokana na kutengana na mme wake aliyemwachia watoto saba.
Hata hivyo mwalimu huyo baada ya kumfanyia ukatili huo  alimficha ndani bila matibabu huku akijitahidi kufanya siri ili majirani wasijue lakini mwisho wa siku waligungua baada ya kuwapo kwa harufu kutokana na vidole vya mikono kuoza na baadhi ya vingine kukatika.
Kitendo cha majirani kugundua tukio hilo kiliwafanya kutoa taarifa Kituo cha Polisi Igogo na kukamatwa lakini kutokana na mme wake kuwa askari hatua zozote hazikuweza kuchukuliwa.
Mtoto Elfrida alichukuliwa na kituo cha kuokoa watoto waliofanyiwa ukatili cha Foundation Karibu Tanzania (FKT) kwa ajili ya matibabu huku wakitarajia jeshi la polisi kuchukua hatua lakini mwisho wa siku hakuna hatua zilizochukuliwa  juu ya tukio hilo.
Hadi sasa tukio hilo halijafikishwa mahakamani kutokana na kile kinachodaiwa ni upelelezi unaendelea lakini ni dhahiri kuna hali ya kulindani
Kibaya zaidi wakati mtoto huyo anatibiwa  katika Hospitali ya Sengerema hadi aliporudishwa Mwanza kwenye kituo cha FKT, walezi hao yaani Mwalimu Miti na askari Kasendela hawakuweza kufika kumjulia hali au kumchukua .
Kitendo cha walezi hao ambao ni watumishi wa Serikali kumtekeleza mtoto huyo kimewafanya FKT kupelekea kesi Tume ya Haki za Binadamu Kanda ya Ziwa Februari Mwaka huu ili kuhakikisha haki inapatikana.
Kutokana na hali hiyo MTANZANIA ilitembelea kituo cha FKT kuona hali ya mtoto huyo pamoja na kufanya mahojiano na viongozi wa kituo hicho ambapo ilishuhudiwa watoto zaidi ya 25  waliofanyiwa ukatili akiwamo Elfrida  wakilelewa hapo.
Ndani ya kituo hicho, MTANZANIA ilishuhudia baadhi ya watoto  wakiwa wamefanyiwa ukatili wa kuchomwa mikono, miguu, kichwa, tumbo, midomo , sehemu za siri,  kuchomwa kisu, kipigo sehemu mbalimbali  za miili yao kama picha zinavyoonekana.
Sababu zilizoelezwa na viongozi wa kituo hicho, ni kwamba watoto hao wamefanyiwa ukatili kutokana na kuiba fedha, kukojoa kitandani, kula mboga, tabia mbaya, uvivu, kuwa na kiburi na vitu vya namna hiyo.
Hakika kituo hicho kinaonekana wazi kuwa kimbilio la watoto wanaoteswa na wazazi na hata Serikali imekuwa ikichukua takwimu za mwaka watoto waliopokelewa hapo kwa kufanyiwa ukatili.
Akizungumza na MTANZANIA, Mratibu Mkuu wa FTK, David Othiambo anasema kwamba vitendo vya ukatili dhidi ya watoto hufanywa na wazazi wao lakini asilimia 90 hufanywa na mama mzazi.
Anasema kuwa kasi ya ukatili wa watoto wadogo unashika kasi Kanda ya Ziwa lakini kwa upande wa upande wa Jiji la Mwanza, Wilaya ya Nyamagana inaongoza kwani kwa wiki wanapokea watoto watatu hadi wanne waliofanyiwa ukatili wa kutisha.
Anasema kwa idadi hiyo kwa mwezi wanapokea watoto 16 ambapo kwa mwaka wanaokoa zaidi ya watoto 201 watoto  ambao wamefanyiwa ukatili wa namna mbalimbali.
Othiambo anasema kundi la watoto wanaofanyiwa ukatili ni kati ya umri siku moja hadi miaka 12 ambao ni waathirika wakubwa na kuongeza kwamba kituo kinapata shida kutokana na jamii kutokuwa tayari kutoa taarifa na kujua suala la kulinda haki za watoto ni la wote.
Anasema licha ya kuwapo na vyombo vya kisheria lakini bado havijafikia hatua ya kutenda haki hasa kwa wale viongozi na watu wenye fedha pale wanafanya ukatili dhidi ya watoto.
imefikia hatua ya wazazi kubaka watoto wao lakini kutokana na kutojua chombo cha kuwatetea wamekuwa wakibaki bila msaada wowote hadi pale anapojitokeza msamaria mwema kitoa taarifa.
Othiambo anasema asilimia 90 watoto alionao kituoni wamefanyiwa ukatili na wazazi wao kwa kupigwa na kuchomwa,  asilimia tatu wamepakwa na asilimia 7 wamenyanyaswa au kunyanyapaliwa.

0683608958
MWISHO.

No comments:

Post a Comment